As Sa'd maelezo
Kwa jina la Mwenyeezi Mungu Mwingi wa Rehema Mwenye Kurehemu
Maelezo: Suuratus Sa'd

Utangulizi:

Rudi kwenye sura

* 1. S'ad: Ni harufi iliyo anzia Sura hii kama zilivyo anzia baadhi ya Sura nyengine kwa mpango wa Qur'ani katika kuanzia kwa harufi moja moja. Naapa kwa Qur'ani yenye utukufu na shani kubwa kuwa hakika hii ni Kweli isiyo na shaka yoyote.
Rudi kwenye sura

* 2. Lakini walio kufuru wamo katika majivuno, hawataki kufuata Haki, na wanawafanyia inda watu wa Haki.
Rudi kwenye sura

* 3. Mataifa mengi tuliyateketeza kabla yao, wakapiga kelele kutaka msaada ilipo wafikia adhabu. Lakini huo haukuwa wakati wa kuiepuka adhabu.
Rudi kwenye sura

* 4. Na walistaajabu watu hawa kuwa amewajia Mtume binaadamu kama wao, na wakasema hao wanao upinga Ujumbe wake: Huyu ni mdanganyifu, mwongo.
Rudi kwenye sura

* 5. Ati amewafanya miungu yote kuwa ni Mungu mmoja tu! Ama hakika jambo hili ni la ajabu, mwisho wa kustaajabisha.
Rudi kwenye sura

* 6. Wakubwa wao wakakimbilia kuusiana wao kwa wao wakiambiana: Endeleeni na njia yenu hiyo hiyo, na shikilieni kuiabudu miungu yenu. Kwani hakika tumepangiwa jambo kubwa hili.
Rudi kwenye sura

* 7. Hatujapata kusikia haya mambo ya Tawhidi, kumfanya Mungu mmoja tu, katika dini ya baba zetu tulio wawahi kuwaona. Haya si chochote ila ni uwongo tu ulio zuliwa.
Rudi kwenye sura

* 8. Basi katika sote sisi, amechaguliwa Muhammad tu peke yake kupewa hishima ya kuteremshiwa Qur'ani?
Rudi kwenye sura

* 9. Bali sisi tunawauliza hawa wanao kuhusudu: Kwani wao wanazo khazina za rehema ya Mola wako Mlezi Mwenye nguvu, Mwingi wa kutoa, hata wao wawe ndio wa kuteua nani wa kumpa Unabii kwa mujibu wa mapenzi ya nafsi zao?
Rudi kwenye sura

* 10. Tena tunawauliza: Kwani wao wanao ufalme wa mbingu na ardhi na viliomo baina yao? Ikiwa hivyo basi nawazipande ngazi mpaka wafikie pahala ambapo watakuwa wakitoa hukumu kama watakavyo, kama wanaweza!
Rudi kwenye sura

* 11. Hao ni askari wanyonge walio shindwa, hapana hivi wala hivi, kama walivyo shindwa mfano kama wao walio jikusanya kuwapinga Manabii.
Rudi kwenye sura

* 12,13. Kabla ya hawa, walikadhibisha kaumu ya Nuhu, kina A'adi na Firauni aliye kuwa na majengo makubwa yaliyo simama imara kama milima, na kina Thamudi na Kaumu Lut'i na Kaumu ya Shuaibu, na watu wa Machakani, kwenye miti mingi iliyo shikamana. Hao ndio walio jumuika kuwapinga Mitume wao kama walivyo jumuika watu wako.
Rudi kwenye sura

* 12,13. Kabla ya hawa, walikadhibisha kaumu ya Nuhu, kina A'adi na Firauni aliye kuwa na majengo makubwa yaliyo simama imara kama milima, na kina Thamudi na Kaumu Lut'i na Kaumu ya Shuaibu, na watu wa Machakani, kwenye miti mingi iliyo shikamana. Hao ndio walio jumuika kuwapinga Mitume wao kama walivyo jumuika watu wako.
Rudi kwenye sura

* 14. Hapana mmoja katika hao wote ila alimkadhibisha Mtume wake, na kwa hivyo ikawashukia adhabu yangu.
Rudi kwenye sura

* 15. Na hao walio jiunga kuwapinga Mitume hawangojei ila ukelele mmoja usio hitajia kukaririwa.
Rudi kwenye sura

* 16. Na makafiri husema kwa kejeli: Mola wetu Mlezi! Tuhimizie sehemu yetu ya adhabu kabla ya Siku ya Malipo.
Rudi kwenye sura

* 17. Ewe Muhammad! Yastahamilie hayo wanayo yasema juu yako washirikina. Na mkumbuke mja wetu, Daudi, mwenye nguvu katika Dini na dunia. Hakika yeye alikuwa mwingi wa kurejea kwa Mwenyezi Mungu katika hali zote.
Rudi kwenye sura

* 18. Hakika Sisi tuliidhalilisha milima pamoja naye, yeye akichuma manufaa kutoka humo, na hiyo milima ikimtakasa Mwenyezi Mungu Mtukufu na kila upungufu, wakati wa mwisho wa mchana na mwanzo wake.
Rudi kwenye sura

* 19. Na pia tukamdhalilishia ndege walio kusanywa kutokana na kila namna na kila pahali. Vyote hivyo, milima na ndege, vikimwitikia Daudi kama atakavyo, akivisarifu kama apendavyo kwa maslaha ya umma.
Rudi kwenye sura

* 20. Tukautia nguvu ufalme wake, na tukampa Unabii na kupambanua baina ya Haki na baat'ili.
Rudi kwenye sura

* 21. Ewe Muhammad! Ati imekujia khabari ya makhasimu wagombanao, walio mjia Daudi kwa kupindukia kuta za mihrabuni palipo kuwa pahala pake pa ibada? Hawakupita mlangoni.
Rudi kwenye sura

* 22. Walipo muingilia Daudi, naye akawaogopa, akababaika. Wakasema: Usikhofu kitu. Sisi ni wenye kuzozana, tumedhulumiana. Basi tuhukumu kwa uadilifu wala usiupindukie huo uadilifu. Na tuongoze kwenye njia iliyo sawa sawa.
Rudi kwenye sura

* 23. Mmoja wa hao wagombanao alisema: Hakika huyu ndugu yangu anao kondoo wa kike tisiini na tisa, na mimi ninaye kondoo mmoja tu. Akasema: Nache niwe nakuchungia kama ninavyo wachunga wangu. Na akanishinda katika usemi.
Rudi kwenye sura

* 24. Daudi akasema kabla hajasikia maneno ya yule mwenye ugomvi mwengine: Hakika huyo amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako amchanganye na wale wake. Na hakika wengi wenye kushirikiana hudhulumiana wao kwa wao, isipo kuwa wale ambao Imani yao imetulia katika nyoyo zao, na wakawa wanatenda mema. Na watu kama hao ni wachache, shida kupatikana. Na Daudi akajua kuwa jambo hili si chochote ila ni mtihani tuliyo mfanyia Sisi. Basi akaomba msamaha kwa Mwenyezi Mungu, na akainama kurukuu kwa Mwenyezi Mungu, na akarejea kwa Mwenyezi Mungu kwa unyenyekevu.
Rudi kwenye sura

* 25. Na Sisi tukamsamehe kule kufanya haraka ya kutoa hukumu. Na hali yeye ana hadhi na marejeo mazuri kwetu.
Rudi kwenye sura

* 26. Na Mwenyezi Mungu alimfunulia kwa kumwambia: Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya wewe uwe Khalifa, yaani Naibu, wetu katika ardhi. Basi wahukumu watu kwa sharia niliyo kupa, wala usiendeshe hukumu kufuata matamanio yao, yakakupotosha njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika wendao pogo na njia ya Mwenyezi Mungu kwa kufuata matamanio yao wao watapata adhabu kali kwa kughafilika kwao na Siku ya Malipo.
Rudi kwenye sura

* 27. Wala Sisi hatukuziumba mbingu na ardhi na viliomo baina yao kwa mchezo. Hayo ndiyo wanayo yadhania makafiri. Na kwa hivyo wakapitisha hukumu kwa mujibu wa pumbao zao. Basi hao walio kufuru watapata adhabu kali ya Moto.
Rudi kwenye sura

* 28. Inaelekeana vipi na hikima yetu na uadilifu wetu tuwafanye sawa baina ya Waumini wenye kutenda mema, na wale wanao fanya uharibifu katika ardhi? Au yaelekea vipi tuwaweke sawa baina ya wenye kuikhofu adhabu yetu na wakaiogopa ikabu yetu na wale walio waasi wakenda kinyume na hukumu zetu?
Rudi kwenye sura

* 29. Ewe Muhammad! Hichi tulicho kuteremshia ni Kitabu chenye manufaa mengi, ili wenye akili nzuri na nyoyo za kufahamu wapate kuzielewa Aya zake, na wawaidhike kwazo.
Rudi kwenye sura

* 30. Na Daudi tulimtunukia mwana, aitwaye Suleiman, mwenye kustahiki sifa nzuri, ambaye anafaa kuitwa, "Mja mwema kweli". Kwa sababu yeye alikuwa mwingi mno wa kurejea kwa Mwenyezi Mungu katika kila hali.
Rudi kwenye sura

* 31. Na hebu taja katika khabari za Suleiman kuwa alipelekewa alasiri farasi wa asli ambao hutulia wanapo simama, na huenda mbio wanapo kwenda.
Rudi kwenye sura

* 32. Suleiman akasema: Hakika mimi nimenyweshwa mapenzi ya farasi, kwa sababu hawa ni katika matayarisho ya mambo ya kheri, nayo ni Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu. Mapenzi haya yametokana na kumkumbuka Mola wangu Mlezi. Na hakusita kushughulika kuwaangalia mpaka wakapotea machoni mwake.
Rudi kwenye sura

* 33. Akaamrisha warudishwe tena kwake apate kujua hali yao. Akaingia kuwapapasa miundi ya miguu yao na shingo zao kwa upole na mapenzi juu yao.
Rudi kwenye sura

* 34. Na hakika Sisi tulimfanyia mtihani Suleiman ili asighurike na heba ya ufalme. Tukaweka juu ya kiti chake kiwiliwili kisicho weza kuendesha mambo. Akautambua mtihani, akarejea kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na akatubu.
Rudi kwenye sura

* 35. Suleiman alimwomba Mola wake Mlezi kwa kurejea kwake: Mola wangu Mlezi! Nighufirie yaliyo toka kwangu kwa ghafla, na unitunukie ufalme usio elekea yeyote kuupata baada yangu. Hakika Wewe ndiye Mwingi wa kutunukia, na ndiye Mwingi wa kutoa.
Rudi kwenye sura

* 36. Tukamdhalilishia upepo, ukenda kama anavyo taka maridhawa, kokote aliko kusudia na kutaka.
Rudi kwenye sura

* 37. Na tukamdhalilishia kila mjenzi na mpiga mbizi katika bahari kuu miongoni mwa mashetani maasi.
Rudi kwenye sura

* 38. Na wengine katika hao mashetani wamefungwa wao kwa wao kwa minyororo, kuwazuia na wenginewe wasifanye ufisadi wao.
Rudi kwenye sura

* 39. Na akamfunulia kwa wahyi : Haya tuliyo kuneemesha kwayo ni kipawa kilicho toka kwetu. Yaani ni Sisi tulio kupa. Basi mpe umtakaye, na mnyime umtakaye. Hapana hisabu juu yako kwa kutoa au kunyima.
Rudi kwenye sura

* 40. Hakika Suleiman kwetu Sisi ana ukaribisho mkubwa, na marejeo mazuri.
Rudi kwenye sura

* 41. Ewe Muhammad! Mkumbuke mja wetu Ayubu alipo mwomba Mola wake Mlezi kwa kusema: Hakika Shetani amenipatisha taabu na machungu.
Rudi kwenye sura

* 42. Tukamuitikia na tukamwambia: Ipige ardhi kwa mguu wako, yatatimbuka maji baridi, utakoga na utakunywa hayo, na kwa hivyo yatakuondokea machofu na adhabu.
Rudi kwenye sura

* 43. Tukamkusanyia watu wake walio kuwa wametapanyika mbali naye siku zile za mateso yake. Na tukamzidishia wenginewe kama wale. Na tulifanya hayo kuwa ni rehema kutokana nasi, na ili yawe ni mawaidha kwa wenye akili, wapate kujua kuwa matokeo ya subira ni faraji.
Rudi kwenye sura

* 44. Ayubu alikuwa kaapa kuwa atampiga mmoja wapo katika ahali zake fimbo kadhaa wa kadhaa. Mwenyezi Mungu alimhalalishia aondoe kiapo chake kwa kuchukua kifungu cha fimbo idadi ile ile alio apia kuwa atampigia. Basi kwa kile kifungu cha fimbo ampige aliye apa kuwa atampiga, na hapo yamini yake itakuwa imetimia kwa uchache wa machungu. Mwenyezi Mungu ndiye aliye mneemesha kwa neema hizi, kwa sababu Mwenyezi Mungu alimwona kuwa ni mtu aliye vumilia masaibu yake. Kwa hivyo amestahiki sifa. Mbora wa kusifiwa kwa ibada ni yeye, kwa sababu yeye ni mwingi mno wa kurejea kwa Mwenyezi Mungu katika kila jambo.
Rudi kwenye sura

* 45. Na mkumbuke mja wetu Ibrahim, na Is-haqa, na Yaa'qubu, wenye nguvu katika Dini na dunia, na wenye busara ya mwangaza.
Rudi kwenye sura

* 46. Hakika Sisi tumewakhusisha wao kwa sifa, nayo ni kuwa wanaikumbuka Nyumba ya Akhera, wao wanaikumbuka nao wanakumbukwa kwayo.
Rudi kwenye sura

* 47. Na hakika wao kwetu Sisi ni wenye kukhitariwa walio bora.
Rudi kwenye sura

* 48. Na mkumbuke Ismail, na Alyasaa, na Dhalkifli - na wote hao ni miongoni mwa walio bora.
Rudi kwenye sura

* 49. Haya tuliyo kusimulia ni khabari za baadhi ya Mitume ili kukukumbusha wewe na kuwakumbusha watu wako. Na hakika wachamngu walio jikinga na kumuasi Mwenyezi Mungu Mtukufu watapata marejeo mazuri na natija njema.
Rudi kwenye sura

* 50. Wameandaliwa bustani za milele zilizo funguliwa milango yao hapana wa kuwazuia wasiingie humo.
Rudi kwenye sura

* 51. Watakuwa wamekaa humo wakiegemea juu ya makochi na vitanda kama wafanyavyo wenye taanusi, wakistarehe kwa kutaka matunda ya kila namna na vinywaji.
Rudi kwenye sura

* 52. Na huko Peponi watakuwa na wake ambao macho yao hayawatazami ila waume zao tu, hawawaangalii wengineo, nao ni wa miaka sawa na waume zao. Kwa hivyo wameelekeana kuwafikiana.
Rudi kwenye sura

* 53. Raha hii ndiyo mliyo ahidiwa kuipata Siku ya Kiyama.
Rudi kwenye sura

* 54. Hakika haya bila ya shaka ni tunayo yatoa Sisi, na wala hayana ukomo.
Rudi kwenye sura

* 55. Neema hizi ni malipo ya wachamngu. Na hakika majabari wenye kuwaasi Manabii wao bila ya shaka watakuwa na marejeo na mwisho muovu.
Rudi kwenye sura

* 56. Na mwisho huo ni Jahannamu watakayo iingia, na moto wake uwatese. Na malalio maovu mno hayo!
Rudi kwenye sura

* 57. Haya maji ya moto, mwisho wa umoto, na usaha wa watu wa Jahannamu wataamrishwa wayaonje.
Rudi kwenye sura

* 58. Na adhabu nyengine mfano wa hizi, za namna kwa namna zilizo changanyika.
Rudi kwenye sura

* 59. Na majabari, wale marais wa washirikina, wataambiwa: Hawa chungu ya watu wanao ingia Motoni pamoja nanyi kwa kusukumana na kwa shida, ni wafwasi wenu. Wale marais watasema: Hawana mapokezi mema hao! Hakika hao wanaingia Motoni wapate kuteseka kwa mvukuto wake.
Rudi kwenye sura

* 60. Na wafwasi hao watasema: Bali nyinyi ndio mnastahiki zaidi hayo maapizo mnayo tuapizia sisi, kwani nyinyi ndio mlio tuletea adhabu hii kwa vile mlivyo tudanganya na mkatuitia ukafirini, nasi tukakufuru kwa sababu yenu. Basi nyumba ovu kabisa ya kukaa ni Jahannamu!
Rudi kwenye sura

* 61. Wafwasi watasema: Ewe Mola wetu Mlezi! Aliye kuwa ni sababu ya adhabu hii, mzidishie adhabu mara mbili katika Moto.
Rudi kwenye sura

* 62. Na watu wa Motoni watasema: Mbona hatuwaoni wale watu ambao tulikuwa duniani tukiwahisabu kuwa ndio katika waovu, na wa duni, wasio kuwa na jema lolote? Na watu hao ni wale mafakiri wa Kiislamu.
Rudi kwenye sura

* 63. Imekuwaje kuwa sisi tukiwakejeli na wala hawakuingia Motoni pamoja nasi? Au wamekwisha ingia na macho yetu yakazibwa tusiwaone tu?
Rudi kwenye sura

* 64, Hakika hayo tuliyo yataja ya hadithi ya watu wa Motoni ni kweli ambayo haina budi kutokea, nayo ni ya kugombana kwa watu wa Motoni wao kwa wao.
Rudi kwenye sura

* 65. Ewe Muhammad! Waambie washirikina: Hakika mimi ni mwenye kukuonyeni na adhabu ya Mwenyezi Mungu, na hapana wa kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu Mmoja ambaye hana mshirika wake, Mtenda nguvu, Mwenye kumshinda kila mwenye madaraka.
Rudi kwenye sura

* 66. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na viliomo baina yao, Mwenye nguvu asiye shindika, Mwenye kusamehe, akazifuta dhambi za mwenye kumuamini.
Rudi kwenye sura

* 67,78. Ewe Muhammad! Waambie: Haya ninayo kuambieni ni khabari kubwa, ambazo nyinyi mnazipuuza. Msizikanye!
Rudi kwenye sura

* 67,78. Ewe Muhammad! Waambie: Haya ninayo kuambieni ni khabari kubwa, ambazo nyinyi mnazipuuza. Msizikanye!
Rudi kwenye sura

* 69. Mimi sikuwa nikijua khabari za watukufu walio juu walipo kuwa wakizozana juu ya shauri ya Adam, kwa sababu mimi sikupitia njia za kupata ilimu zilizo zowewa na watu za kusoma vitabu au kupokea masomo kwa wataalamu. Njia yangu mimi ya kujua ni kwa kufunuliwa kwa Wahyi.
Rudi kwenye sura

* 70. Na mimi sikufunuliwa kwa Wahyi ila kwamba hakika mimi ni Mtume wa kukufikishieni Ujumbe wa Mola wangu Mlezi kwa njia iliyo wazi kabisa.
Rudi kwenye sura

* 71. Watajie pale alipo sema Mola wako Mlezi kuwaambia Malaika: Mimi nataka umba mtu, naye ni Adam a.s., kutokana na udongo.
Rudi kwenye sura

* 72. Nikisha timiza kumuumba na nikampulizia siri ya uhai, nayo ni roho, muangukieni kwa kusujudu sijida ya kumtukuza na kumuamkia.
Rudi kwenye sura

* 73,74. Malaika wote wakafanya kama walivyo amrishwa, wakamuangukia wakisujudu, isipo kuwa Iblisi. Yeye hakusujudu, na akajiona bora na akapanda kiburi, na akawa miongoni mwa makafiri.
Rudi kwenye sura

* 73,74. Malaika wote wakafanya kama walivyo amrishwa, wakamuangukia wakisujudu, isipo kuwa Iblisi. Yeye hakusujudu, na akajiona bora na akapanda kiburi, na akawa miongoni mwa makafiri.
Rudi kwenye sura

* 75. Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema: Ewe Iblisi! Nini kilicho kuzuilia kumsujudia niliye muumba Mimi mwenyewe bila ya kuingiliwa na yeyote kati yake! Umejiona mkubwa hali nawe si mkubwa, au hakika wewe nafsi yako ni katika walio shinda ukubwa?
Rudi kwenye sura

* 76. Iblisi akasema: Mimi ni bora kuliko Adam; kwani Wewe umeniumba kwa moto, na yeye umemuumba kwa udongo. Basi vipi mimi nimsujudie yeye?
Rudi kwenye sura

* 77. Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa kumlipa Iblisi kwa kiburi chake cha kukataa amri ya Mola wake Mlezi, alimwambia: Basi toka kwenye kundi la watukufu walio juu, kwani wewe umekwisha fukuzwa kutokana na rehema yangu!
Rudi kwenye sura

* 78. Na hakika wewe umetengwa mbali na kila kheri mpaka Siku ya Malipo. Hapo utalipwa kwa sababu ya kunikufuru Mimi na kunifanyia kiburi.
Rudi kwenye sura

* 79. Iblisi akasema: Mola Mlezi! Nipe muhula, wala usinifishe mpaka Siku ya kufufuliwa viumbe.
Rudi kwenye sura

* 80,81. Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Basi wewe utaakhirishwa, utapewa muhula, mpaka siku ya wakati tunao ujua Sisi, nao ni kumalizika dunia.
Rudi kwenye sura

* 80,81. Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Basi wewe utaakhirishwa, utapewa muhula, mpaka siku ya wakati tunao ujua Sisi, nao ni kumalizika dunia.
Rudi kwenye sura

* 82,83. Iblisi akasema: Basi naapa kwa Ukubwa wako na Utukufu wako, kwa yakini nitawapoteza watu wote, isipo kuwa waja wako ulio wateuwa kwa ajili ya kukut'ii Wewe. Hao sina madaraka nao.
Rudi kwenye sura

* 82,83. Iblisi akasema: Basi naapa kwa Ukubwa wako na Utukufu wako, kwa yakini nitawapoteza watu wote, isipo kuwa waja wako ulio wateuwa kwa ajili ya kukut'ii Wewe. Hao sina madaraka nao.
Rudi kwenye sura

* 84,85. Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Haki ndiyo yamini yangu na kiapo changu; na wala sisemi ila Haki. Bila ya shaka nitaijaza Jahannamu kwa jinsi yako ya kishetani na watakao kufuata katika vizazi vya Adam wote. Hapana khitilafu kwangu baina ya wafuasi na wanao fuatwa.
Rudi kwenye sura

* 84,85. Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Haki ndiyo yamini yangu na kiapo changu; na wala sisemi ila Haki. Bila ya shaka nitaijaza Jahannamu kwa jinsi yako ya kishetani na watakao kufuata katika vizazi vya Adam wote. Hapana khitilafu kwangu baina ya wafuasi na wanao fuatwa.
Rudi kwenye sura

* 86. Ewe Muhammad! Waambie umma wako: Mimi sikuombeni ujira kwa ajili ya haya niliyo amrishwa nikufikishieni yaliyomo katika Qur'ani na Wahyi. Wala mimi si katika hao wanao jipamba na yasiyo kuwa yao, hata nijidai Unabii.
Rudi kwenye sura

* 87. Haikuwa Qur'ani ila ni ukumbusho na mawaidha kwa walimwengu wote.
Rudi kwenye sura

* 88. Na hapana shaka nyinyi, mnao ikadhibisha Qur'ani, mtakuja jua karibuni hivi ukweli uliomo ndani yake wa ahadi, na maonyo, na khabari za mambo yatakayo kuja, na Ishara za ulimwengu.
Rudi kwenye sura

Copyright © 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al Barwani