Azzukhruf maelezo
Kwa jina la Mwenyeezi Mungu Mwingi wa Rehema Mwenye Kurehemu
Maelezo: Suuratul Azzukhruf

Utangulizi:

Rudi kwenye sura

* 1. H'a Mim:- Imeanza Sura hii kwa baadhi ya harufi za kutamkwa kama ilivyo ada ya Qur'ani katika kuanzishia Sura nyingi kwa harufi kama hizi.
Rudi kwenye sura

* 2. Mwenyezi Mungu, Subhanahu, anaapa kwa Qur'ani inayo eleza wazi yale iliyo yakusanya katika mambo ya itikadi na hukumu.
Rudi kwenye sura

* 3. Hakika Sisi tumeijaalia Qur'ani iwe kwa lugha ya Kiarabu, ili mweze kuelewa umuujiza wake, na mweze kuzingatia maana zake.
Rudi kwenye sura

* 4. Na hakika hii Qur'ani iliyo thibiti katika Lauhun Mahfuudh, Ubao ulio hifadhiwa, ulioko kwetu, bila ya shaka, ina cheo cha juu, na imepangwa kwa mpango wa hikima, katika mwisho wa ufasihi. (Vitabu vyote vya mbinguni asili yake anayo Mwenyezi Mungu, katika Ujuzi wake wa tokea azali, Al- I'lmu al-azaliy au Ubao Ulio Hifadhiwa Al-lauhu al-mahfuudh au Asili ya Maandiko Ummu-l-kitabi. Kwa sababu ya kuwa Vitabu vilivyo kuja zamani, ikiwa Taurati, Zaburi, Injili n.k. vilikuwa ni vya muda fulani, na kwa mataifa fulani, basi haikuwepo dharura vibaki kwa usafi kila neno lake. Ni makusudio yake tu yabakie, yaliyo kuwa ya msingi. Ama ulipo fika wakati wa kudumisha Ujumbe wa Mwenyezi Mungu kwa zama zote, na kwa watu wote, ndio ikaja Qur'ani ambayo imehifadhiwa kila neno lake. Na ndio siri ya kuletwa kwa lugha ya Kiarabu na ikalindwa kwa lugha ile, ijapo kuwa itatarajumiwa katika lugha nyengine. Mzozano wowote unao tokea unarejezwa kwenye asli ile ya Kiarabu ambayo haikubadilika hata chembe, wala haitabadilika mpaka Siku ya Kiyama. Huo peke yake ni muujiza. Ama vitabu vya Biblia ni kama maji yaliyo tibuliwa na ng'ombe mpaka kwenye chemchem yake. Chemchem ya Qur'ani haikutibuliwa. Ijapo kuwa wanyama na watu wanaweza kunywa maji yake huku chini, kwenye kitovu cha chemchem hakuguswi. Huko ni kwenye Qur'ani hiyo ya Kiarabu, safi kama ilivyo kwenye Ubao Ulio Hifadhiwa.)
Rudi kwenye sura

* 5. Je! Tukupeni muhula, tuache kukuteremshieni Qur'ani kwa kukutupilieni mbali, kwa sababu ya kupita kwenu mipaka ya ukafiri juu ya nafsi zenu? Hayawi hayo, kwa kufuata hukumu ya kulazimikana kwenu na hoja.
Rudi kwenye sura

* 6. Nasi tuliwatuma Manabii wengi kuyaendea mataifa yaliyo tangulia, basi hapana ajabu kitu kumtuma Mtume kwenu.
Rudi kwenye sura

* 7. Wala hawajii Mtume yeyote kuwakumbusha Haki ila huendelea na kumfanyia maskhara.
Rudi kwenye sura

* 8. Basi tuliwateketeza walio kadhibisha walio tangulia; na hao walikuwa wamewazidi makafiri wa Makka kwa nguvu na ushupavu. Basi wasidanganyike hawa na ujabari wao. Na zilikwisha tangulia katika Qur'ani hadithi za ajabu za watu wa kale, za kuwafanya wenginewe wazingatie. Basi enyi mnao kanusha! Zingatieni!
Rudi kwenye sura

* 9. Na ninaapa, ewe Mtume! Ukiwauliza makafiri nani aliye ziumba mbingu na ardhi? Bila ya shaka watasema kuyajibu hayo: Mwenyezi Mungu ndiye aliye ziumba, ambaye anasifika kwa hakika ya mambo kuwa ni Mwenye nguvu, na Mwenye Ujuzi ulio enea.
Rudi kwenye sura

* 10. Ambaye amekufanyieni ardhi ni pahala palipo tanda, ili muweze kukaa humo na mjitumilie, na akakufanyieni ndani yake njia mnazo zipitia katika safari zenu mpate kufikia mtakako.
Rudi kwenye sura

* 11. Na ambaye aliye kuteremshieni maji kwa kiasi ya haja kutoka mbinguni tukaihuisha nchi kavu isiyo na mimea. Kuhuisha kama huko ndivyo mtavyo fufuliwa kutoka makaburini kwenu kwa ajili ya hisabu. Basi yawaje mnakukataa?
Rudi kwenye sura

* 12. Na ambaye aliye kuumbieni namna zote za viumbe, akavifanya vikutumikieni vyombo vya baharini na ngamia kuwa ni vipando katika safari zenu kutimiza haja zenu.
Rudi kwenye sura

* 13. Ili mtulie juu yao, kisha mkumbuke neema za Muumba wenu na Mlezi wenu kwa kuvifanya hivyo vikutumikieni mnapo tulia juu yao, na kwa kuadhimisha kule kuvifanya vinyonge kwa njia ya ajabu, na kutambua uweza mlio wezeshwa kuvidhibiti na kuvitawala, mseme: Subhana, Ametakasika aliye mfanya huyu (au hichi) kuwa dhalili kututumikia na sisi wenyewe tusingeli weza kumdhalilisha.
Rudi kwenye sura

* 14. Na hakika sisi ni wenye kurejea kwa Muumba wetu baada ya maisha haya, ili ahisabiwe kila mmoja kwa iliyo tanguliza mikono yake.
Rudi kwenye sura

* 15. Na makafiri washirikina wamemfanyia Mwenyezi Mungu Subhanahu katika viumbe vyake mwana wakaamini kuwa ni sehemu ya nafsi yake. Hakika mwanaadamu kwa kitendo chake hichi hadi amepita ukomo katika ukafiri wake, na upinzani wake uwazi.
Rudi kwenye sura

* 16. Ati mnadai kwamba Yeye amejitwalia katika viumbe vyake watoto wa kike, na nyinyi akakukhiarieni watoto wanaume? Ama hakika haya ni mambo ya ajabu kweli!
Rudi kwenye sura

* 17. Wamekuzulia Wewe hayo, na ilhali wao akipewa khabari mmoja wao kwamba amepata mtoto wa kike uso wake husawajika kwa kuudhika, naye kajaa masikitiko na huzuni kwa kuona anapewa khabari mbaya.
Rudi kwenye sura

* 18. Hivyo hawa wana fanya jeuri ya kumpachikia Mwenyezi Mungu mwana, ambaye kwa maumbile yake amelelewa katika mapambo, na hata hawezi kujadiliana na kupambana kwa hoja kwa nuksani yake ya kubaini. Ama hili ni jambo la ajabu!
Rudi kwenye sura

* 19. Na ati wakawaita Malaika, viumbe vya Mwenyezi Mungu, kuwa ni wanawake. Kwani wao waliwashuhudia walipo umbwa, hata watoe hukumu kwa jambo hilo? Hawakuliona! Sisi tutausajili uzushi wao huu. Na Siku ya Kiyama watakuja hisabiwa.
Rudi kwenye sura

* 20. Na washirikina husema ati: Lau kuwa Mwingi wa Rehema angeli kuwa anataka tusiiabudu hii miungu basi tusingeli iabudu. Wanakusudia kudai kuwa ati Mwenyezi Mungu yu radhi kuabudiwa hiyo miungu. Wanasema hayo bila ya kuwa na ilimu yoyote ya kuyategemezea wayasemayo. Hawa si chochote ila ni wenye kudhani tu. Hunena maneno yasio na ushahidi wowote.
Rudi kwenye sura

* 21. Kwani tuliwapa Kitabu kabla ya Qur'ani cha kuunga mkono huu uzushi wao, ndio maana wakashikamana nao kwa nguvu hivi? Hatukuwateremshia Kitabu namna hiyo. Basi hawana hoja ya kuinukulu.
Rudi kwenye sura

* 22. Lakini washirikina walipo shindwa na hoja zote walisema: Hakika sisi tumewakuta baba zetu wakifuata dini hii; na sisi tunaendelea kufuata nyayo zao.
Rudi kwenye sura

* 23. Mfano wa hali ya watu hawa ni mfano wa mataifa yaliyo tangulia. Hatukumtuma Mtume yeyote kwenye mji kabla yako ila walisema wale wenye kuneemeka katika huo mji, nao ndio walio takabari kwa hizo neema: Hakika sisi tumewakuta baba zetu wakifuata dini hii, basi ndio sisi tunakwenda mwendo wao. Basi kufuata kijinga ni upotovu wa tangu kale.
Rudi kwenye sura

* 24. Mwonyaji akasema: Je! Mnafuata baba zenu hata nikikujieni na yaliyo elekea zaidi kukupelekeni kwenye uwongofu kuliko mlio wakuta nao baba zenu? Wakasema kuwajibu Mitume wao wakiwakadhibisha kwa Dini: Sisi tunayakataa yote mliyo tumwa kutuambia!
Rudi kwenye sura

* 25. Basi tukawatesa walio wakadhibisha Mitume wao kwa mateso makali katika dunia. Basi hebu angalia, ewe mwenye kuzingatia, vipi ulikuwa mwisho wa wenye kukukadhibisheni kuwa ni mfano wa ajabu, na mawaidha makubwa!
Rudi kwenye sura

* 26. Na ewe Muhammad! Waambie hao wanao kanusha hadithi ya Ibrahim pale alipo mwambia baba yake: Hakika mimi nimejitenga mbali na ibada ya kuiabudu hii miungu yenu ya uwongo.
Rudi kwenye sura

* 27. Lakini mimi namuabudu Mwenyezi Mungu aliye niumba; kwani ni Yeye ndiye atakaye niongoza kwendea Njia ya Haki.
Rudi kwenye sura

* 28. Kwa kuwatangazia hivyo, likawa hilo Neno la Tawhidi, ni neno lenye kubakia katika dhuriya zake, ili wapate kulirejelea, waliamini.
Rudi kwenye sura

* 29. Washirikina hawakutimiza matumaini ya Ibrahim, wala Mimi sikuwapatiliza papo kwa papo, bali nimewastarehesha hawa ulio nao, ewe Muhammad, na niliwastarehesha baba zao kabla yao kwa namna mbali mbali za neema, mpaka ilipo teremka Qur'ani kuwaitia Haki, na akawajia Mtume mwenye kubaini wazi akiwaita.
Rudi kwenye sura

* 30. Na ilipo teremka Qur'ani kuwaongoza kwenye Tawhid wakaongeza juu ya ushirikina wao kuita Qur'ani : "uchawi" na "kiini macho", kwa kejeli. Na wakashikilia ukafiri wao.
Rudi kwenye sura

* 31. Na washirikina, kwa kumdharau Muhammad na kuona haiwezi kuwa yeye ateremshiwe Qur'ani, walisema: Kwa nini basi hii Qur'ani, ambayo yeye anadai kuwa ni Wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, asiteremshiwe mtu mkubwa mtukufu katika watu wa Makka au T'aif?
Rudi kwenye sura

* 32. Funguo za Utume hazimo katika mikono ya washirikina, hata wao wawakabidhi watu wenye vyeo. Sisi tumewapangia maisha yao kwa kuwa wao wenyewe hawajiwezi. Na tumewafadhilisha baadhi juu ya wengine katika riziki na vyeo, na kwa hivyo baadhi yao huwafanya wengineo wawasaidie na wawatumikie katika kutimiza haja zao, ili wategemeane katika kutafuta maisha na kupanga uhai. Na Unabii na yaliyo khusiana nayo katika neema za Akhera na dunia, ni bora kuliko vyeo vyote vya duniani.
Rudi kwenye sura

* 33. Na lau kuwa si karaha ya kuwa watu wote wawe makafiri wakiona makafiri wamo katika nafasi ya riziki, basi tungeli wafanyia wanao mkufuru Mwenyezi Mungu kuwa nyumba zao ziwe na dari za fedha, na pia ngazi za nyumba zao, kwa kuwa hayo hayana thamani kitu mbele yetu.
Rudi kwenye sura

* 34,35. Na tungeli wafanyia milango ya nyumba zao na vitanda kuwa ni vya fedha wakineemeka navyo na wakiegemea juu yake. Na tungeli wafanyia mapambo ya kila kitu. Na starehe zote hizo tulizo kusifia si chochote ila ni starehe za kupita njia, ni za uhai huu tu wa duniani. Na malipo ya Akhera mbele ya Muumba wako na Mlezi wako yameandaliwa kwa wanao jilinda na ushirikina, na wakayaepuka maasi ya kuangamiza.
Rudi kwenye sura

* 34,35. Na tungeli wafanyia milango ya nyumba zao na vitanda kuwa ni vya fedha wakineemeka navyo na wakiegemea juu yake. Na tungeli wafanyia mapambo ya kila kitu. Na starehe zote hizo tulizo kusifia si chochote ila ni starehe za kupita njia, ni za uhai huu tu wa duniani. Na malipo ya Akhera mbele ya Muumba wako na Mlezi wako yameandaliwa kwa wanao jilinda na ushirikina, na wakayaepuka maasi ya kuangamiza.
Rudi kwenye sura

* 36. Na mwenye kujitia upofu na Qur'ani aliyo iteremsha Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema kuwa ni kumbusho kwa walimwengu wote, tunamsalitisha na Shetani, anakuwa naye daima, akimpoteza na akimzuzua.
Rudi kwenye sura

* 37. Na hakika Mashetani wanao jitia upofu na Qur'ani huwazuia na Njia anayo itia Rahmani. Na hao wanao tumiliwa wanadhani kwa kuwafuata rafiki zao kwamba wao wamo katika uwongofu.
Rudi kwenye sura

* 38. Hata yule aliye jipa upofu na Qur'ani atapo fika kwa Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama, na akaona matokeo ya kule kujitia kwake upofu, atamwambia rafiki yake kwa majuto: Laiti wewe nami tungeli kuwa mbali mbali duniani umbali wa mashariki na magharibi! Ama wewe ulikuwa sahibu muovu mno kwangu, mpaka umekuja nitumbukize katika shimo la Motoni!
Rudi kwenye sura

* 39. Na hapo wataambiwa kwa kuwahizi: Leo hamtapunguziwa adhabu, kwani mmejidhulumu wenyewe kwa ukafiri wenu, kwa sababu mlishirikiana na mashetani wenu. Kwani kila mmoja anateseka kwa adhabu ya kumtosha mwenyewe.
Rudi kwenye sura

* 40. Je! Unaweza kumwongoa aliye pita mipaka katika upotovu? Je! Unaweza kumfanya asikie aliye kiziwi hasikii la kweli, kipofu hazingatii, na ambaye katika ujuzi wa Mwenyezi Mungu atakufa katika upotovu? Huwezi hayo! Kwa sababu hao wamekwisha thibiti katika ukafiri wao, basi hawanafiiki kwa wanayo yasikia, wala wanayo yaona.
Rudi kwenye sura

* 41. Basi tukikushika tukakufisha kabla hatuja kuonyesha adhabu yao, na kifua chako kikatua kwa hayo, na pia vifua vya Waumini, alaa kulli hali, Sisi bila ya shaka tutawaadhibu duniani na Akhera.
Rudi kwenye sura

* 42. Au unataka tukuonyeshe adhabu tuliyo waahidi kabla ya kufa kwako, tutakuonyesha, kwani Sisi tunawaweza hao kwa uweza wetu na nguvu zetu.
Rudi kwenye sura

* 43. Ikiwa moja ya mawili haya lazima liwe bila ya shaka, basi shikamana na Qur'ani tuliyo kufunulia, na simama imara katika kuitekeleza, kwani hakika wewe uko katika Njia ya Haki Iliyo Nyooka.
Rudi kwenye sura

* 44. Na hakika hii Qur'ani ni utukufu mkubwa juu yako, ewe Muhammad, na wa Umma wako, kwa kuwa umeteremshiwa kwa lugha ya Kiarabu, na mtakuja kuhojiwa Siku ya Kiyama juu ya haki yake, na shukrani za neema zake.
Rudi kwenye sura

* 45. Na hebu angalia katika sharia za Mitume wetu tulio watuma kabla yako. Ati umekuja humo wito wa kuwaita watu wende kuabudu vitu visio kuwa Mwenyezi Mungu? Haukuja! Basi hao wanao abudu asiye kuwa Mwenyezi Mungu mmoja hadi wamepita mipaka katika upotovu wao!
Rudi kwenye sura

* 46. Na bila ya shaka Sisi tulimtuma Musa tukampa miujiza yenye kuthibitisha ukweli wake, ende kwa Firauni na watu wake. Akasema: Hakika mimi ni Mtume wa Muumba wa walimwengu wote na Mlezi wao nimetumwa kwenu. Wakamtaka aonyeshe miujiza.
Rudi kwenye sura

* 47. Alipo wajia kwa miujiza ya kuthibitisha Utume wake mara wakampokea kwa kumcheka, na kumfanyia tashtiti, na kumcheza shere, bila ya kuzingatia maneno yake.
Rudi kwenye sura

* 48. Na kila muujiza katika miujiza iliyo wajia mfululizo, kwa uwazi wa hoja zake juu ya ukweli wa Mtume, na kuwa kila mmoja peke yake unatimiza makusudio hayo kwa ukamilifu wa kila njia, na ukamilifu wa nafsi yake, hata ukiuangalia waweza kusema: Muujiza huu ni mkubwa kuliko ule mwengine. Na walipo shikilia kuendelea na uasi tuliwapatiliza kwa balaa za namna kwa namna, ili warejee, waache upotovu wao.
Rudi kwenye sura

* 49. Wakasema, kumlilia Musa balaa zilipo waenea: Ewe mchawi - ndio Mwanachuoni kikwao - Tuombee kwa Mola wako Mlezi, kwa kutawasali na ahadi yake aliyo kupa, atuondolee adhabu hii! Hakika sisi tukifarijiwa bila ya shaka tutaongoka.
Rudi kwenye sura

* 50. Mwenyezi Mungu alipo waondolea masaibu yale kwa kuitikia dua za Musa, wakamshitukia kwa kuvunja ile ahadi yao ya kuamini.
Rudi kwenye sura

* 51. Firauni akawatangazia watu wake kutangaza nguvu zake na madaraka yake: Kwani huu ufalme wa Misri si wangu mimi peke yangu, wala hapana mwenginewe, na hii mito ambayo mnaiona inapita chini ya jumba langu? Hamyaoni haya? Basi hamzingatii mnayo yaona ya nguvu zangu na udhaifu wa Musa? Na Firauni alitaka kwa wito wake kuutia imara ut'iifu wao.
Rudi kwenye sura

* 52. Firauni akasema akizidisha ujabari: Bali mimi ni bora kuliko dhaifu huyu mnnyonge, asiye weza hata kubainisha wazi huo wito wake kwa ulimi wa fasaha.
Rudi kwenye sura

* 53. Akazidi kusema kuchochea kumkadhibisha Musa: Lau ingeli kuwa Mola wake Mlezi angeli mvika vikuku vya dhahabu kwa kumpa funguo za utawala, au akamsaidia kwa Malaika wa kumuunga mkono, ingeli kuwa yeye ni mkweli katika madai yake ya Utume?
Rudi kwenye sura

* 54. Firauni akawa anawachochea watu wake, na akawaathiri kwa udanganyifu huu, nao wakamt'ii katika upotovu wake. Kwani hao walikuwa watu walio kwisha toka kwenye Dini ya Mwenyezi Mungu Iliyo Nyooka.
Rudi kwenye sura

* 55. Basi walipo tughadhibisha hadi ya kutughadhibisha, kwa kupita kwao mipaka ya ufisadi, tuliwaangamiza kwa kuwazamisha wote.
Rudi kwenye sura

* 56. Tukamfanya Firauni na kaumu yake kuwa ni viongozi wa makafiri wa baada yao katika kustahiki mfano wa adhabu yao, na kuwa ni masimulizi ya namna ya ajabu ya watu wote kuyazingatia.
Rudi kwenye sura

* 57. Na alipo pigiwa mfano Isa bin Maryam katika kuwa kwake kama Adam kwa kuwa Mwenyezi Mungu alimuumba kwa udongo, kisha akamwambia: Kuwa, na akawa, s.l. Basi yeye ni mtumwa aliye umbwa, aliye neemeshwa kwa kupewa Unabii, s.l. Haifai kumuabudu badala ya Mwenyezi Mungu. Na watu wako wanapuuza hizo sifa zinazo pigiwa mfano, na wala hawafahamu.
Rudi kwenye sura

* 58. Makafiri wamesema: Je! Miungu yetu na Isa, nani bora? Ikiwa yeye yuko Motoni basi sisi na miungu yetu tutakuwa pamoja naye. Hawakupigii mfano huu wewe ila kutafuta ubishi tu, na kushindana kwa maneno, si kwa ajili ya kuitafuta kweli ilivyo. Bali hawa ni watu ambao ni shadidi wa khasama, wamebobea kwa hayo.
Rudi kwenye sura

* 59. Isa si chochote ila ni mja tuliye mneemesha kwa kumpa Unabii, na tumemfanya awe ni zingatio la ajabu kama ni mithali, kwa kumuumba bila ya baba, kwa Wana wa Israili, wapate ushahidi wa ukamilifu wa uweza wetu.
Rudi kwenye sura

* 60. Na lau tungeli taka, tungeli wageuza baadhi yenu, enyi watu, mkawa ni Malaika mkifuatana katika ardhi, kama wanavyo kufuateni watoto wenu, mjue kwamba Malaika wananyenyekea kufuata kudra ya Mwenyezi Mungu. Basi vipi wao wastahiki Ungu?
Rudi kwenye sura

* 61. Na hakika Isa kwa kuzuka kwake bila ya baba, na kuponyesha kwake vipofu na wakoma ni dalili ya kukaribia Saa ya Kiyama. Basi usiwe na shaka nayo. Na fuateni uwongofu wangu na Mtume wangu. Hii ninayo kuitieni ndiyo Njia Iliyo Nyooka yenye kufikilia Uwokovu.
Rudi kwenye sura

* 62. Wala asikuzuilieni Shetani kuifuata Njia Iliyo Nyooka. Hakika huyo ni adui aliye dhaahiri uadui wake.
Rudi kwenye sura

* 63. Na alipo tumwa Isa kwa Wana wa Israili naye ana miujiza iliyo wazi, na Ishara zenye kubainisha, aliwaambia: Nimekujieni na sharia yenye hikima nzuri, inayo kuiteni muifuate Tawhidi (Imani ya Mwenyezi Mungu Mmoja). Na nimekujieni nikubainishieni baadhi ya mambo mnayo khitalifiana kwayo katika mambo ya Dini ili mpatane kwenye Haki. Basi iogopeni adhabu ya Mwenyezi Mungu, na mnit'ii mimi katika hayo ninayo kuitieni.
Rudi kwenye sura

* 64. Hakika Mwenyezi Mungu, peke yake, ndiye Muumba wangu, na ni Muumba wenu, basi muabuduni Yeye pasi mwenginewe. Na ihafidhini sharia yake. Hii ninayo kuitieni muifuate ni Njia Iliyo Nyooka itakayo kufikisheni kwenye uwokovu.
Rudi kwenye sura

* 65. Makundi mbali mbali yakakhitalifiana baina ya Wakristo baada ya Isa, kwa kufarikiana juu yake. Maangamizo yatawafika hao walio dhulumu kwa waliyo yasema juu ya Isa ya ukafiri, watapata adhabu kali na chungu Siku ya Kiyama.
Rudi kwenye sura

* 66. Makafiri hawangojei kitu baada ya kuipuuza Imani ila kuwafikia Saa kwa ghafla, nao wameghafilika nayo.
Rudi kwenye sura

* 67. Marafiki walio kusanyika duniani kwa upotovu, watakuwa maadui wao kwa wao siku itakapo wafikia Saa kwa ghafla, na yatakatika mapenzi yote, ila mapenzi ya wenye kuogopa, nao wangali duniani, kuiogopa adhabu ya Mwenyezi Mungu, na wakashikamana huko duniani katika kumt'ii Yeye.
Rudi kwenye sura

* 68. Mwenyezi Mungu atawaambia wachamngu kwa kuwafanyia hishima: Enyi waja wangu! Leo msikhofu adhabu yoyote, wala msihuzunike. Mmekwisha salimika na adhabu. Na Mwenyezi Mungu amekudhaminieni thawabu.
Rudi kwenye sura

* 69. Walio ziamini Ishara za Mwenyezi Mungu na wakamt'ii Yeye, na wakawa wanamnyenyekea.
Rudi kwenye sura

* 70. Siku ya Kiyama wataambiwa kwa kufanyiwa hishima: Ingieni Peponi, nyinyi na wake zenu, nanyi mmo katika furaha iliyo kubwa, ambayo itadhihiri kwenye nyuso zenu.
Rudi kwenye sura

* 71. Na baada ya kuingia Peponi watakuwa wakizungukiwa kwa sahani za dhahabu, na bilauri kadhaalika, na humo watapata vyakula namna mbali mbali, na vinywaji vya kila namna. Na humo Peponi watapata kila kitamaniacho moyo, na kituzacho macho. Na kukamilisha furaha wataambiwa: Nyinyi mtakaa milele katika neema hizi.
Rudi kwenye sura

* 72. Na kutimiza neema, wataambiwa: Hii ndiyo Pepo mliyo ipata kwa sababu ya vitendo vyema mlivyo vitanguliza mlipo kuwa duniani.
Rudi kwenye sura

* 73. Humo mtapata matunda ya namna nyingi, na kwa wingi, mtastarehe kuyala.
Rudi kwenye sura

* 74. Hakika walio tenda makosa kwa ukafiri watakuwamo katika adhabu ya Jahannamu daima dawamu.
Rudi kwenye sura

* 75. Hawapunguziwi adhabu wakosefu hawa, wala haisitishwi, na wao watakata tamaa ya kuokoka.
Rudi kwenye sura

* 76. Wala Sisi hatukuwadhulumu wakosefu hawa kwa adhabu hii, lakini wao wenyewe ndio walio jidhulumu nafsi zao kwa kukhiari upotofu kuliko uwongofu.
Rudi kwenye sura

* 77. Na wakosefu, watapo kwisha kata tamaa ya kupunguziwa adhabu kali, watamwita Malik, huyo ni askari wa Motoni wakimwambia: Mwombe Mola wako Mlezi atufishe tupumzike na adhabu ya Jahannamu. Na Malik awambie: Nyinyi mtakaa humu humu katika adhabu milele!
Rudi kwenye sura

* 78. Mwenyezi Mungu Mtukufu atawaambia kwa kuwarudi: Nyinyi alikujilieni Mtume wetu, enyi watu wa Makka, kukuleteeni Dini ya Haki. Wakaamini wachache, na wengi wenu mkakataa. Nao hawaipendi Haki.
Rudi kwenye sura

* 79. Kwani ndio waliweza washirikina wa Makka kutimiza hivyo vituko vyao kumkadhibisha Mtume na kupanga njama za kumuuwa? Bali Sisi kwa hakika tuliweza jambo katika kuwalipizia wao na kukupa ushindi wewe juu yao.
Rudi kwenye sura

* 80. Ati wanadhani hawa washirikina kwamba Sisi hatuyasikii maneno yao wenyewe wanapo panga njama, na wanapo semezana kwa siri katika kukanusha haki? Kwani! Twawasikia. Na Malaika wanao dhibiti kauli zao wanayaandika hayo.
Rudi kwenye sura

* 81. Waambie hao washirikina: Ikithibitika kwa ushahidi kuwa kweli Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema ana mwana, basi mimi ningeli kuwa wa kwanza kumuabudu mwana huyo. Lakini hayo hayakuthibiti kwa hoja yoyote kwamba Rahmani ana mwana, kwa kuwa hayo ni kumfanya Mwenye nguvu awe hajiwezi, Mwenye kujitosha awe mhitaji. Na Yeye, Subhanahu, ametakasika na kila la upungufu kwa ukamilifu wake.
Rudi kwenye sura

* 82. Ametakasika kwa mtakasiko wa Mwenye kuziumba mbingu na ardhi na A'rshi Tukufu, kwa yote wanayo msifia washirikina, ambayo hayaelekeani na Ungu wake.
Rudi kwenye sura

* 83. Basi waachilie wazame katika upotovu wao, na wacheze katika dunia yao, wayaache mambo yenye maana, wala wasiyashughulikie, mpaka iwajie Siku ya Kiyama waliyo ahidiwa, ipate kila nafsi kulipwa kwa iliyo yachuma.
Rudi kwenye sura

* 84. Na Yeye ndiye anaye abudiwa mbinguni kwa haki, na anaabudiwa katika ardhi kwa haki. Na Yeye, peke yake, ndiye Mwenye hikima za mwisho katika vitendo vyake na mipango yake, Mwenye kujua kila kitu kilicho kuwa na kitakacho kuwa.
Rudi kwenye sura

* 85. Na ametukuka na ametaadhamu Yeye ambaye, peke yake, Mwenye ukamilifu wa kutekeleza katika mbingu na ardhi na baina yao katika viumbe vya angani vinavyo onekana na vyenginevyo, na mipango yote iko kwake, na Yeye tu ndiye Mwenye kujua wakati wa Kiyama, na kwake Yeye peke yake, mtarejeshwa mwishoe kwa ajili ya hisabu.
Rudi kwenye sura

* 86. Na hio miungu yao wanayo iabudu badala ya Mwenyezi Mungu haimiliki uweza wa kuwaombea hao wanao waabudu. Lakini wenye kushuhudia kwa Tawhidi, yaani hao wanao amini ya kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mola wao Mlezi kwa haki, hao wanaweza kuombewa miongoni mwa Waumini atakao Mwenyezi Mungu kuwaombea.
Rudi kwenye sura

* 87. Na ewe Mtume! Ukiwauliza hawa washirikina nani aliye waumba, bila ya shaka watasema: Kawaumba Mwenyezi Mungu. Basi inakuwaje wakaacha kumuabudu Mwenyezi Mungu Mtukufu wakenda kuwaabudu wenginewe, nao wanakiri kuwa Yeye ndiye Muumba wao? Ama hakika jambo hili ni la ajabu!
Rudi kwenye sura

* 88. Naapa kwa kauli ya Muhammad s.a.w. anapo omba na kuita: Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika hawa wenye inda ni watu wasio tarajiwa kuamini.
Rudi kwenye sura

* 89. Basi waachilie mbali, ewe Mtume, kwa wingi wa inda yao, na waambie: Langu mimi nikukuacheni kwa salama yenu kutoka kwangu, na salama yangu kutoka kwenu. Nanyi mtakuja jua kuwa mwisho wa inda yao ni khasara iliyo wazi.
Rudi kwenye sura

Copyright © 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al Barwani