5.Suurat Al-Maida |
Imeshuka Madina | Ina aya 120 |
Utangulizi | Orodha ya Sura | Faharasa |
KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
0
1. Enyi mlio amini! Timizeni ahadi. Mmehalalishiwa wanyama wa mifugo,
ila wale mnao tajiwa. Lakini msihalalishe kuwinda nanyi mmo katika Hija.
Hakika Mwenyezi Mungu anahukumu apendavyo.
1
2. Enyi mlio amini! Msivunje hishima ya alama ya Dini ya Mwenyezi
Mungu wala mwezi mtakatifu, wala wanyama wanao pelekwa Makka kuchinjwa,
wala vigwe vyao, wala wanao elekea kwendea Nyumba Takatifu, wakitafuta
fadhila na radhi za Mola wao Mlezi. Na mkisha toka Hija yenu basi windeni.
Wala kuwachukia watu kwa kuwa wali- kuzuilieni kufika Msikiti mtakatifu
kusikupelekeeni kuwafanyia uadui. Na saidianeni katika wema na uchamngu.
Wala msisaidiane katika dhambi na uadui. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika
Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
2
3. Mmeharimishiwa nyamafu, na damu, na nyama ya nguruwe, na mnyama
aliye chinjwa si kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na aliye kufa kwa kunyongeka
koo, na aliye kufa kwa kupigwa, na aliye kufa kwa kuanguka, na aliye kufa
kwa kupigwa pembe, aliye liwa na mnyama, ila mkimdiriki kumchinja. Na pia
ni haramu kula nyama aliye chinjiwa masanamu. Na ni haramu kupiga ramli.
Hayo yote ni upotovu. Leo walio kufuru wamekata tamaa na Dini yenu; basi
msiwaogope, bali niogopeni Mimi. Leo nimekukamiliishieni Dini yenu, na
nimekutimizieni neema yangu, na nimekupendeleeni UISLAMU uwe ndiyo Dini.
Na mwenye kushurutishwa na njaa, bila ya kupendelea dhambi, basi hakika
Mwenyezi Mungu ni Msamehevu na Mwenye kurehemu.
3
4. Wanakuuliza wamehalalishiwa nini? Sema: Mmehalalishiwa kila vilivyo
vizuri na mlicho wafundisha wanyama kukiwinda. Mnawafundisha alivyo kufunzeni
Mwenyezi Mungu. Basi kuleni walicho kukamatieni, na mkisomee jina la Mwenyezi
Mungu. Na mcheni Mwenyezi Mungu; hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.
4
5. Leo mmehalalishiwa kila vilivyo vizuri. Na chakula cha walio pewa
Kitabu ni halali kwenu, na chakula chenu ni halali kwao. Na pia wanawake
wema miongoni mwa Waumini, na wanawake wema miongoni mwa walio pewa Kitabu
kabla yenu, mtakapo wapa mahari yao, mkafunga nao ndoa, bila ya kufanya
uhasharati wala kuwaweka kinyumba. Na anaye kataa kuamini bila shaka a'mali
yake imepotea, naye katika Akhera atakuwa miongoni mwa wenye khasara.
5
6. Enyi mlio amini! Mnapo simama kwa ajili ya Sala basi osheni nyuso
zenu, na mikono yenu mpaka vifundoni, na mpake vichwa vyenu, na osheni
miguu yenu mpaka vifundoni. Na mkiwa na janaba basi ogeni. Na mkiwa wagonjwa
au mmo safarini, au mmoja wenu ametoka chooni au mmewagusa wanawake, na
hamkupata maji, basi tayamamuni vumbi lilio safi, na mpake nyuso zenu na
mikono yenu. Hapendi Mwenyezi Mungu kukutieni katika taabu; bali anataka
kukutakaseni na kutimiza neema yake juu yenu ili mpate kushukuru.
6
7. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu, na ahadi
yake aliyo fungamana nanyi mlipo sema: Tumesikia na tumet'ii. Na mcheni
Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi sana wa yaliyomo vifuani.
7
8. Enyi mlio amini! Kuweni wasimamizi madhubuti kwa ajili ya Mwenyezi
Mungu mkitoa ushahidi kwa haki. Wala kuchukiana na watu kusikupelekeeni
kutofanya uadilifu. Fanyeni uadilifu. Hivyo ndio kuwa karibu mno na uchamngu.
Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu anazo khabari za mnayo
yatenda.
8
9. Mwenyezi Mungu amewaahidi walio muamini na wakatenda mema kwamba
watapata maghfira na malipo makubwa.
9
10. Na wale walio kufuru na wakakanusha Ishara zetu, hao ndio watu
wa Motoni.
10
11. Enyi mlio amini! Kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu zilizo juu
yenu, walipo taka watu kukunyooshieni mikono, naye akaizuilia mikono yao
kukufikieni. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Na Waumini wamtegemee Mwenyezi Mungu
tu.
11
12. Na Mwenyezi Mungu alifanya agano na Wana wa Israili. Na tukawateulia
kutokana nao wakuu kumi na mbili. Na Mwenyezi Mungu akasema: Kwa yakini
Mimi ni pamoja nanyi. Mkisali, na mkatoa Zaka, na mkawaamini Mitume wangu,
na mkawasaidia, na mkamkopesha Mwenyezi Mungu mkopo mwema, hapana shaka
nitakufutieni maovu yenu na nitakuingizeni katika mabustani yapitayo mito
kati yake. Lakini atakaye kufuru miongoni mwenu baada ya hayo bila ya shaka
atakuwa amepotea njia iliyo sawa.
12
13. Basi kwa sababu ya kuvunja agano lao tuliwalaani, na tukazifanya
nyoyo zao kuwa ngumu. Wanayabadilisha maneno kutoka pahala pake, na wamesahau
sehemu ya yale waliyo kumbushwa. Na huachi kuvumbua khiana kutokana nao,
isipo kuwa wachache miongoni mwao. Basi wasamehe na waache. Hakika Mwenyezi
Mungu huwapenda wafanyao wema.
13
14. Na kutoka kwa wale walio sema: Sisi ni Manasara, tulichukua ahadi
yao, lakini wakasahau sehemu ya waliyo kumbushwa. Kwa hivyo tukaweka kati
yao uadui na chuki mpaka Siku ya Kiyama. Na hapo Mwenyezi Mungu atawaambia
waliyo kuwa wakiyafanya.
14
15. Enyi Watu wa Kitabu! Amekwisha kujieni Mtume wetu anaye kufichulieni
mengi mliyo kuwa mkiyaficha katika Kitabu, na anaye samehe mengi. Bila
shaka imekujieni kutoka kwa Mwenyezi Mungu nuru na Kitabu kinacho bainisha.
15
16. Mwenyezi Mungu huwaongoa wenye kufuata radhi yake katika njia
za salama, na huwatoa katika giza kuwapeleka kwenye nuru kwa amri yake,
na huwaongoa kwenye njia iliyo nyooka.
16
17. Hakika wamekufuru walio sema: Mwenyezi Mungu ni Masihi mwana
wa Maryamu. Sema: Ni nani mwenye kumiliki cho chote mbele ya Mwenyezi Mungu
ikiwa Yeye angetaka kumuangamiza Masihi mwana wa Maryamu, na mama yake,
na wote waliomo katika ardhi? Na mamlaka ya mbingu na ardhi na vilivyomo
ndani yake ni vya Mwenyezi Mungu. Huumba apendavyo. Na Mwenyezi Mungu anao
uweza juu ya kila kitu.
17
18. Na Mayahudi na Wakristo wanasema: Sisi ni wana wa Mwenyezi Mungu
na vipenzi vyake. Sema: Basi kwa nini anakuadhibuni kwa ajili ya dhambi
zenu? Bali nyinyi ni watu tu kama wale wengine alio waumba. Humsamehe amtakaye
na humuadhibu amtakaye. Na ni wa Mwenyezi Mungu tu ufalme wa mbingu na
ardhi. Na marejeo ni kwake Yeye.
18
19. Enyi Watu wa Kitabu! Bila ya shaka amekujilieni Mtume wetu akikubainishieni
katika wakati usio kuwa na Mitume, msije mkasema: Hakufika kwetu mbashiri
wala mwonyaji. Basi amekujieni mbashiri na mwonyaji. Na Mwenyezi Mungu
anao uweza wa kila kitu.
19
20. Na pale Musa alipo waambia watu wake: Enyi watu wangu! Kumbukeni
neema za Mwenyezi Mungu zilizo juu yenu, alipo wateuwa Manabii kati yenu,
na akakufanyeni watawala, na akakupeni ambayo hakuwapa wowote katika walimwengu.
20
21. Enyi watu wangu! Ingieni katika nchi takatifu ambayo Mwenyezi
Mungu amekuandikieni. Wala msirudi nyuma, msije mkawa wenye kukhasirika.
21
22. Wakasema: Ewe Musa! Huko wako watu majabari. Nasi hatutaingia
huko mpaka wao watoke humo. Wakitoka humo hapo tutaingia.
22
23. Watu wawili miongoni mwa wachamngu ambao Mwenyezi Mungu amewaneemesha,
walisema: Waingilieni kwa mlangoni. Mtakapo waingilia basi kwa yakini nyinyi
mtashinda. Na mtegemeeni Mwenyezi Mungu ikiwa nyinyi ni Waumini.
23
24. Wakasema: Ewe Musa! Sisi hatutaingia humo kamwe maadamu wao wamo
humo. Basi nenda wewe na Mola wako Mlezi mkapigane. Sisi tutakaa hapa hapa.
24
25. Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi similiki ila nafsi yangu
na ndugu yangu. Basi tutenge na hawa watu wapotovu.
25
26. (Mwenyezi Mungu) akasema: Basi nchi hiyo wameharimishiwa muda
wa miaka arubaini, watakuwa wakitanga-tanga katika ardhi. Basi wewe usiwasikitikie
watu wapotovu.
26
27. Na wasomee khabari za wana wawili wa Adam kwa kweli. Walipo toa
mhanga, ukakubaliwa wa mmoja wao, na wa mwengine haukukubaliwa. Akasema:
Nitakuuwa. Akasema mwengine: Mwenyezi Mungu huwapokelea wachamngu.
27
28. Ukininyooshea mkono wako kuniuwa, mimi sitakunyooshea mkono wangu
kukuuwa. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.
28
29. Mimi nataka ubebe dhambi zangu na dhambi zako, kwani wewe utakuwa
miongoni mwa watu wa Motoni. Na hayo ndiyo malipo ya wenye kudhulumu.
29
30. Basi nafsi yake ikampelekea kumuuwa nduguye, akamuuwa na akawa
miongoni mwa wenye kukhasirika.
30
31. Hapo Mwenyezi Mungu akamleta kunguru anaye fukua katika ardhi
ili amwonyeshe vipi kumsitiri nduguye. Akasema: Ole wangu! Nimeshindwa
kuwa kama kunguru huyu nikamsitiri ndugu yangu? Basi akawa miongoni mwa
wenye kujuta.
31
32. Kwa sababu ya hayo tuliwaandikia Wana wa Israili ya kwamba aliye
muuwa mtu bila ya yeye kuuwa, au kufanya uchafuzi katika nchi, basi ni
kama amewauwa watu wote. Na mwenye kumuokoa mtu na mauti ni kama amewaokoa
watu wote. Na hakika waliwajia Mitume wetu na hoja zilizo wazi. Kisha wengi
katika wao baada ya haya wakawa waharibifu katika nchi.
32
33. Basi malipo ya wale wanao mpiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake
na wakawania kufanya uchafuzi katika nchi, ni kuuwawa, au kusalibiwa, au
kukatwa mikono yao na miguu yao kwa mabadilisho, au kutolewa nchi. Hii
ndiyo hizaya yao katika dunia; na katika Akhera watapata adhabu kubwa.
33
34. Isipo kuwa wale walio tubu kabla hamjawatia nguvuni. Na jueni
kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira na Mwenye kurehemu.
34
35. Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na tafuteni njia ya kumfikilia.
Na wanieni kwa juhudi kwa ajili yake ili mpate kuokoka.
35
36. Hakika walio kufuru lau wange kuwa na yote yaliyomo duniani,
na mengine kama hayo, ili watoe fidia ya kuepukana na adhabu ya Siku ya
Kiyama, yasingeli pokelewa kwao; na watapata adhabu chungu.
36
37. Watataka watoke Motoni, lakini hawatatoka humo, na watakuwa na
adhabu inayo dumu.
37
38. Na mwizi mwanamume na mwizi mwanamke, ikateni mikono yao, hayo
ni malipo ya waliyo yachuma, ndiyo adhabu ya mfano itokayo kwa Mwenyezi
Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu na Mwenye hikima.
38
39. Lakini mwenye kutubia baada ya dhulma yake, na akatengenea, basi
Mwenyezi Mungu atapokea toba yake. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira
na Mwenye kurehemu.
39
40. Hujui ya kwamba Mwenyezi Mungu anao ufalme wa mbingu na ardhi?
Humuadhibu amtakaye, na humsamehe amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza
wa kila kitu.
40
41. Ewe Mtume! Wasikuhuzunishe wa fanyao haraka kukufuru, miongoni
mwa wanao sema kwa vinywa vyao: Tumeamini, na hali nyoyo zao hazikuamini,
na miongoni mwa Mayahudi, wanao sikiliza kwa ajili ya uwongo, wanao sikiliza
kwa ajili ya watu wengine wasio kufikia. Wao huyabadilisha maneno kutoka
pahala pake. Wanasema: Mkipewa haya basi yashikeni, na msipo pewa haya
tahadharini. Na mtu ambaye Mwenyezi Mungu anataka kumfitini huwezi kuwa
na madaraka naye mbele ya Mwenyezi Mungu. Hao ndio ambao Mwenyezi Mungu
hataki kuzitakasa nyoyo zao. Watakuwa na hizaya duniani, na Akhera watakuwa
na adhabu kubwa.
41
42. Hao ni wasikilizaji kwa ajili ya kusema uwongo, na ni walaji
mno vya haramu! Basi wakikujia, wahukumu baina yao au jipuuze nao. Na ukijipuuza
nao, basi wao hawatakudhuru kitu. Na ukiwahukumu, basi hukumu baina yao
kwa uadilifu. Hakika Mwenyezi Mungu anawapenda waadilifu.
42
43. Na huwaje wakufanye wewe hakimu nao wanayo Taurati yenye hukumu
za Mwenyezi Mungu? Kisha baada ya hayo wanageuka. Na hao si wenye kuamini.
43
44. Hakika Sisi tuliteremsha Taurati yenye uwongofu na nuru, ambayo
kwayo Manabii walio nyenyekea kiislamu, na wachamngu, na wanazuoni, waliwahukumu
Mayahudi; kwani walikabidhiwa kukihifadhi Kitabu cha Mwenyezi Mungu. Nao
wakawa ni mashahidi juu yake. Basi msiwaogope watu, bali niogopeni Mimi.
Wala msibadilishe Aya zangu kwa thamani chache. Na wasio hukumu kwa aliyo
teremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio makafiri.
44
45. Na humo tuliwaandikia ya kwamba roho kwa roho, na jicho kwa jicho,
na pua kwa pua, na sikio kwa sikio, na jino kwa jino, na kwa majaraha kisasi.
Lakini atakaye samehe basi itakuwa ni kafara kwake. Na wasio hukumu kwa
yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio madhaalimu.
45
46. Na tukawafuatishia hao Isa bin Maryamu kuyahakikisha yaliyo kuwa
kabla yake katika Taurati, na tukampa Injili iliyomo ndani yake uwongofu,
na nuru na inayo sadikisha yaliyo kuwa kabla yake katika Taurati, na uwongofu
na mawaidha kwa wachamngu.
46
47. Na wahukumu Watu wa Injili kwa yale aliyo teremsha Mwenyezi Mungu
ndani yake. Na wasio hukumu kwa yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu basi
hao ndio wapotofu.
474
48. Na tumekuteremshia wewe, kwa haki, Kitabu hichi kinacho sadikisha
yaliyo kuwa kabla yake katika Vitabu na kuyalinda. Basi hukumu baina yao
kwa aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, wala usifuate matamanio yao ukaacha
Haki iliyo kujia. Kila mmoja katika nyinyi tumemwekea sharia yake na njia
yake. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angeli taka ange kufanyeni nyote umma
mmoja, lakini ni kukujaribuni kwa aliyo kupeni. Basi shindaneni kwa mambo
ya kheri. Kwa Mwenyezi Mungu ndio marejeo yenu nyote, na atakuja kuwaambieni
yale mliyo kuwa mkikhitalifiana.
48
49. Na wahukumu baina yao kwa aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, wala
usifuate matamanio yao. Nawe tahadhari nao wasije kukufitini ukaacha baadhi
ya aliyo kuteremshia Mwenyezi Mungu. Na wakigeuka, basi jua kwamba hakika
Mwenyezi Mungu anataka kuwasibu kwa baadhi ya dhambi zao. Na hakika wengi
wa watu ni wapotofu.
49
50. Je, wao wanataka hukumu za Kijahiliya? Na nani aliye mwema zaidi
katika kuhukumu kuliko Mwenyezi Mungu kwa watu wenye yakini?
50
51. Enyi mlio amini! Msiwafanye Mayahudi na Wakristo kuwa ni marafiki.
Wao ni marafiki wao kwa wao. Na miongoni mwenu mwenye kufanya urafiki nao,
basi huyo ni katika wao. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu.
51
52. Utawaona wale wenye maradhi nyoyoni mwao wanakimbilia kwao wakisema:
Tunakhofu yasitusibu mabadiliko. Huenda Mwenyezi Mungu akaleta ushindi
au jambo jingine litokalo kwake wakawa wenye kujuta kwa waliyo yaficha
katika nafsi zao.
52
53. Na walio amini watasema: Hivyo hawa ndio wale walio apa ukomo
wa viapo vyao kuwa wao wa pamoja nanyi? Vitendo vyao vitapotea bure, na
wataamkia kuwa wenye kukhasirika.
53
54. Enyi mlio amini! Atakaye iacha miongoni mwenu Dini yake, basi
Mwenyezi Mungu atakuja leta watu anao wapenda nao wanampenda, wanyenyekevu
kwa Waumini na wenye nguvu juu ya makafiri, wanapigania Jihadi katika Njia
ya Mwenyezi Mungu, wala hawaogopi lawama ya anaye laumu. Hiyo ndiyo fadhila
ya Mwenyezi Mungu, humpa amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mkunjufu na Mwenye
kujua.
54
55. Hakika rafiki yenu mlinzi ni Mwenyezi Mungu na Mtume wake na
walio amini, ambao hushika Sala na hutoa Zaka nao wananyenyekea.
55
56. Na atakaye fanya urafiki na Mwenyezi Mungu na Mtume wake na walio
amini, basi hakika kundi la Mwenyezi Mungu ndilo lenye kushinda.
56
57. Enyi mlio amini! Msiwafanye marafiki wale walio ifanyia kejeli
na mchezo Dini yenu miongoni mwa walio pewa Kitabu kabla yenu, na makafiri
wengine. Na mcheni Mwenyezi Mungu kama nyinyi ni wenye kuamini.
57
58. Na mnapo adhinia Sala wao wanaichukulia maskhara na mchezo. Hayo
ni kwa sababu wao ni watu wasio na akili.
58
59. Sema: Enyi Watu wa Kitabu! Hivyo mnatuchukia kwa kuwa tumemuamini
Mwenyezi Mungu na tuliyo teremshiwa na yaliyo teremshwa kabla, na kwa kuwa
wengi katika nyinyi ni wapotofu?
59
60. Sema: Je! Nikwambieni yule ambaye ni mwenye malipo mabaya zaidi
kuliko hayo mbele ya Mwenyezi Mungu? Ni yule ambaye Mwenyezi Mungu amemlaani
na amemkasirikia, na amewafanya miongoni mwao manyani na nguruwe, na wakamuabudu
Shet'ani. Hao ndio wenye mahali pabaya na wamepotea zaidi njia iliyo sawa.
60
61. Na wanapo kujieni husema: Tumeamini. Lakini hakika wao wameingia
na ukafiri wao, na wametoka nao pia. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi kabisa
wa yote wanayo yaficha.
61
62. Na utawaona wengi katika wao wanakimbilia kwenye dhambi, na uadui,
na ulaji wao vya haramu. Ni maovu mno hayo wayatendayo!
62
63. Mbona hao wanazuoni na makohani wao hawawakatazi maneno yao ya
dhambi, na ulaji wao vya haramu? Ni maovu mno hayo wayafanyayo!
63
64. Na Mayahudi walisema: Mkono wa Mwenyezi Mungu umefumba. Mikono
yao ndiyo iliyo fumba, na wamelaaniwa kwa sababu ya waliyo yasema. Bali
mikono yake iwazi. Hutoa apendavyo. Kwa yakini yaliyo teremshwa kwako kutoka
kwa Mola wako Mlezi yatawazidisha wengi katika wao uasi na kufuru. Na Sisi
tumewatilia uadui na chuki baina yao mpaka Siku ya Kiyama. Kila mara wanapo
washa moto wa vita, Mwenyezi Mungu anauzima. Na wanajitahidi kuleta uharibifu
katika ardhi. Na Mwenyezi Mungu hawapendi waharibifu.
64
65. Na lau kuwa Watu wa Kitabu wangeli amini na wakachamngu hapana
shaka tungeli wafutia makosa yao, na tungeli waingiza katika Bustani zenye
neema.
65
66. Na lau kuwa wangeli ishika Taurati na Injili na yote waliyo teremshiwa
kutokana na Mola wao Mlezi, basi hapana shaka wangeli kula vya juu yao
na vya chini ya miguu yao. Wapo watu miongoni mwao walio sawa, lakini wengi
wao wanayo yafanya ni mabaya mno.
66
67. Ewe Mtume! Fikisha uliyo teremshiwa kutoka kwa Mola wako Mlezi.
Na ikiwa hukufanya hayo basi hukufikisha ujumbe wake. Na Mwenyezi Mungu
atakulinda na watu. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu makafiri.
67
68. Sema: Enyi Watu wa Kitabu! Hamna lenu jambo mpaka muishike Taurati
na Injili na yote mlio teremshiwa kutokana na Mola wenu Mlezi. Na hakika
ulio teremshiwa wewe kutokana na Mola wako Mlezi yatawazidishia wengi katika
wao uasi na ukafiri. Basi usiwasikitikie watu makafiri.
68
69. Hakika walio amini, na Mayahudi na Masabii na Wakristo, walio
muamini Mwenyezi Mungu, na Siku ya mwisho, na wakatenda mema, basi hawatakuwa
na khofu wala hawatahuzunika.
69
70. Tulifanya agano na Wana wa Israili, na tukawatumia Mitume. Kila
alipo wajia Mtume kwa wasio yapenda nafsi zao wengine waliwakanusha na
wengine wakawauwa.
70
71. Na wakadhani kuwa hapatakuwa majaribio; basi wakawa vipofu na
viziwi. Kisha Mwenyezi Mungu akawapokelea toba zao. Kisha tena wengi katika
wao wakawa vipofu na viziwi. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona hayo wayatendayo.
71
72. Hakika wamekufuru walio sema: Mwenyezi Mungu ni Masihi mwana
wa Maryamu! Na hali Masihi mwenyewe alisema: Enyi Wana wa Israili! Muabuduni
Mwenyezi Mungu, Mola wangu Mlezi na Mola wenu Mlezi. Kwani anaye mshirikisha
Mwenyezi Mungu, hakika Mwenyezi Mungu atamharimishia Pepo, na mahala pake
ni Motoni. Na walio dhulumu hawatakuwa na wa kuwanusuru.
72
73. Kwa hakika wamekufuru walio sema: Mwenyezi Mungu ni wa tatu wa
Utatu. Hali hakuna mungu ila Mungu Mmoja. Na ikiwa hawaachi hayo wanayo
yasema, kwa yakini itawakamata adhabu chungu wale wanao kufuru.
73
74. Je! Hawatubu kwa Mwenyezi Mungu na wakamwomba msamaha? Na Mwenyezi
Mungu ni Mwenye maghfira na Mwenye kurehemu.
74
75. Masihi mwana wa Maryam si chochote ila ni Mtume. Wamekwisha pita
Mitume kabla yake. Na mama yake ni mwanamke mkweli. Wote wawili walikuwa
wakila chakula. Angalia jinsi tunavyo wabainishia Aya, kisha angalia vipi
wanavyo geuzwa.
75
76. Sema: Je! Mnawaabudu, badala ya Mwenyezi Mungu, wale ambao hawawezi
kukudhuruni wala kukufaeni? Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kusikia, Mwenye
kujua.
76
77. Sema: Enyi Watu wa Kitabu! Msipite kiasi katika dini yenu bila
ya haki. Wala msifuate matamanio ya watu walio kwisha potea tangu zamani,
na wakawapoteza wengi, na wenyewe wakapotea njia iliyo sawa.
77
78. Walilaaniwa walio kufuru miongoni mwa Wana wa Israili kwa ulimi
wa Daud na wa Isa mwana wa Maryamu. Hayo ni kwa sababu waliasi na wakawa
wanapindukia mipaka.
78
79. Walikuwa hawakatazani maovu waliyo kuwa wakiyafanya. Hakika ni
maovu yalioje mambo waliyo kuwa wakiyafanya!
79
80. Utawaona wengi wao wanafanya urafiki na walio kufuru. Hakika
ni maovu yaliyo tangulizwa na nafsi zao hata Mwenyezi Mungu amewakasirikia,
nao watadumu katika adhabu.
80
81. Na lau wangeli kuwa wanamuamini Mwenyezi Mungu, na huyu Nabii,
na yaliyo teremshwa kwake, wasingeli wafanya hao marafiki. Lakini wengi
katika wao ni wapotofu.
81
82. Hakika utawakuta walio shadidi kuliko watu wote katika uadui
kwa walio amini ni Mayahudi na washirikina. Na utawakuta walio karibu mno
kwa mapenzi ni wale wanao sema: Sisi ni Manasara. Hayo ni kwa sababu wapo
miongoni mwao makasisi na wamonaki, na kwa sababu wao hawafanyi kiburi.
82
83. NA WANAPO SIKIA yaliyo teremshwa kwa Mtume utaona macho yao yanachururika
machozi kwa sababu ya Haki waliyo itambua. Wanasema: Mola wetu Mlezi! Tumeamini.
Basi tuandike pamoja na wanao shuhudia.
83
84. Na kwa nini tusimuamini Mwenyezi Mungu na Haki iliyo tujia, na
hali tunatumai Mola wetu Mlezi atuingize pamoja na watu wema?
84
85. Basi Mwenyezi Mungu atawalipa, kwa yale waliyo yasema, Bustani
zipitazo mito katika yake; humo watadumu. Na haya ndiyo malipo ya wafanyao
wema.
85
86. Na wale walio kufuru na wakazikanusha Ishara zetu, hao ndio watu
wa Motoni.
86
87. Enyi mlio amini! Msiharimishe vizuri alivyo kuhalalishieni Mwenyezi
Mungu, wala msikiuke mipaka. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi wakiukao mipaka.
87
88. Na kuleni katika alivyo kuruzukuni Mwenyezi Mungu, halali na
vizuri. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye mnamuamini.
88
89. Mwenyezi Mungu hatakushikeni kwa viapo vyenu vya upuuzi, lakini
atakushikeni kwa mnavyo apa kweli kweli kwa makusudio. Basi kafara yake
ni kuwalisha masikini kumi kwa chakula cha wastani mnacho walisha ahali
zenu, au kuwavisha, au kumkomboa mtumwa. Asiye pata hayo, basi afunge siku
tatu. Hii ndiyo kafara ya viapo vyenu mnapo apa. Na hifadhini yamini zenu.
Namna hivyo Mwenyezi Mungu anakubainishieni Aya zake ili mpate kushukuru.
89
90. Enyi mlio amini! Bila ya shaka ulevi, na kamari, na kuabudu masanamu,
na kupiga ramli, ni uchafu katika kazi ya Shet'ani. Basi jiepusheni navyo,
ili mpate kufanikiwa.
90
91. Hakika Shet'ani anataka kutia kati yenu uadui na chuki kwa ulevi
na kamari, na akuzuieni kumkumbuka Mwenyezi Mungu na kusali. Basi je, mmeacha?
91
92. Na mt'iini Mwenyezi Mungu, na mt'iini Mtume, na tahadharini.
Na ikiwa mtageuka basi jueni ya kuwa juu ya Mtume wetu ni kufikisha ujumbe
tu ulio wazi.
92
93. Si dhambi juu ya walio amini na wakatenda mema kwa walivyo vila
(zamani) maadamu wakichamngu na wakiamini na wakitenda mema, kisha wakachamngu,
na wakaamini, kisha wakachamngu na wakafanya mazuri. Na Mwenyezi Mungu
huwapenda wafanyao mazuri.
93
94. Enyi mlio amini! Mwenyezi Mungu atakujaribuni kidogo kwa wanyama
wa kuwinda inayo wafikia mikono yenu na mikuki yenu, ili Mwenyezi Mungu
amjue nani anaye mkhofu kwa ghaibu. Basi atakaye ruka mipaka baada ya hayo
atapata adhabu kali.
94
95. Enyi mlio amini! Msiue wanyama wa kuwinda nanyi mmeharimia katika
Hija. Na miongoni mwenu atakaye muuwa makusudi, basi malipo yake yatakuwa
kwa kuchinja kilicho sawa na alicho kiuwa, katika mifugo, kama wanavyo
hukumu waadilifu wawili miongoni mwenu. Mnyama huyo apelekwe kwenye Al
Kaaba, au kutoa kafara kwa kuwalisha masikini; au badala ya hayo ni kufunga,
ili aonje ubaya wa jambo lake hili. Mwenyezi Mungu amekwisha yafuta yaliyo
pita; lakini atakaye fanya tena Mwenyezi Mungu atampa adhabu. Na Mwenyezi
Mungu ndiye Mwenye nguvu na Mwenye kuadhibu.
95
96. Nyinyi mmehalalishiwa kuvua vinyama vya baharini na kuvila, kwa
faida yenu na kwa wasafiri. Na mmeharimishiwa mawindo ya wanyama wa bara
maadamu mmeharimia Hija. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye mtakusanywa kwake.
96
97. Mwenyezi Mungu ameifanya Al Kaaba, hii Nyumba Tukufu, ni simamio
la watu, na kadhaalika Miezi Mitukufu, na wanyama wa dhabihu, na vigwe.
Hayo ili mjue ya kwamba Mwenyezi Mungu anayajua yaliyomo mbinguni na yaliyomo
katika ardhi, na ya kwamba Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.
97
98. Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu, na ya kwamba
Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira, na Mwenye kurehemu.
98
99. Haimlazimu Mtume ila kufikisha ujumbe tu. Na Mwenyezi Mungu anajua
mnacho kidhihirisha na mnacho kificha.
99
100. Sema: Haviwi sawa viovu na vyema ujapo kupendeza wingi wa viovu.
Basi mcheni Mwenyezi Mungu, enyi wenye akili, ili mpate kufanikiwa.
100
101. Enyi mlio amini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatakuchukizeni.
Na mkiyauliza inapo teremshwa Qur'ani mtabainishiwa. Mwenyezi Mungu amesamehe
hayo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira Mpole.
101
102. Waliyauliza hayo watu wa kabla yenu, kisha wakawa wenye kuyakataa.
102
103. Mwenyezi Mungu hakujaalia uharamu wowote juu ya "Bahira" wala
"Saiba" wala "Wasila" wala "Hami". Lakini walio kufuru humzulia uwongo
Mwenyezi Mungu, na wengi wao hawatumii akili.
103
104. Na wanapo ambiwa: Njooni kwenye yale aliyo yateremsha Mwenyezi
Mungu, na kwa Mtume, husema: Yanatutosha tuliyo wakuta nayo baba zetu.
Je, hata ikiwa baba zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?
104
105. Enyi mlio amini! Kilicho lazima juu yenu ni nafsi zenu. Hawakudhuruni
walio potoka ikiwa nyinyi mmeongoka. Ni kwa Mwenyezi Mungu ndio marudio
yenu nyote; basi atakwambieni yale mliyo kuwa mkiyatenda.
105
106. Enyi mlio amini! Yanapo mfikia mauti mmoja wenu na akataka kutoa
wasia, basi wawepo mashahidi wawili miongoni mwenu ambao ni waadilifu.
Na mnapo kuwa safarini, na msiba wa mauti ukakusibuni, basi washuhudie
wengineo wawili wasio kuwa katika nyinyi. Mtawazuia wawili hao baada ya
Sala na waape kwa Mwenyezi Mungu, mkitilia shaka, wakisema: Hatutopokea
thamani yoyote kwa haya hata kwa ajili ya jamaa; na wala hatutaficha ushahidi
wa Mwenyezi Mungu; hakika hapo tutakuwa miongoni mwa wenye dhambi.
106
107. Ikigundulikana kuwa wawili hao wamestahiki dhambi, basi wawili
wengineo kutokana na warithi wenye kudai haki washike makamo ya wa mwanzo.
Nao waape kwa Mwenyezi Mungu wakisema: Hakika ushahidi wetu ni wa haki
zaidi kuliko ushahidi wa wale. Na sisi hatujafanya dhambi; hakika hapo
tutakuwa miongoni mwa walio dhulumu.
107
108. Hivi inaelekea zaidi ya kwamba watatoa ushahidi ulio sawa au
wataogopa visije vikaletwa viapo vingine baada ya viapo vyao. Na mcheni
Mwenyezi Mungu na msikie. Na hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi wapotofu.
108
109. Ile siku ambayo Mwenyezi Mungu atapo wakusanya Mitume awaambie:
Mlijibiwa nini? Watasema: Hatuna ujuzi; hakika Wewe ndiye Mjuzi Mkubwa
wa yote yaliyo fichikana.
109
110. Na pale Mwenyezi Mungu atapo sema: Ewe Isa bin Maryamu! Kumbuka
neema yangu juu yako, na juu ya mama yako, nilipo kutia nguvu kwa Roho
Takatifu, ukazungumza na watu katika utoto na utuuzimani. Na nilivyo kufunza
kuandika na hikima na Taurati na Injili. Na ulipo tengeneza udongo sura
ya ndege, kwa idhini yangu, kisha ukapuliza ikawa ndege kwa idhini yangu;
na ulipo waponesha vipofu na wakoma kwa idhini yangu; na ulipo wafufua
wafu kwa idhini yangu; na nilipo kukinga na Wana wa Israili ulipo wajia
na hoja zilizo wazi, na wakasema walio kufuru miongoni mwao: Haya si lolote
ila ni uchawi mtupu!
110
111. Na nilipo wafunulia Wanafunzi kwamba waniamini Mimi na Mtume
wangu, wakasema: Tumeamini na shuhudia kuwa sisi ni Waislamu.
111
112. Wanafunzi walipo sema: Ewe Isa bin Maryamu! Je, Mola wako Mlezi
anaweza kututeremshia chakula kutoka mbinguni? Akasema: Mcheni Mwenyezi
Mungu ikiwa nyinyi ni Waumini.
112
113. Wakasema: Tunataka kukila chakula hicho, na nyoyo zetu zitue,
na tujue kwamba umetuambia kweli, na tuwe miongoni mwa wanao shuhudia.
113
114. Akasema Isa bin Maryamu: Ewe Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wetu!
Tuteremshia chakula kutoka mbinguni ili kiwe Sikukuu kwa ajili ya wa mwanzo
wetu na wa mwisho wetu, na kiwe ni Ishara itokayo kwako. Basi turuzuku,
kwani Wewe ndiye mbora wa wanao ruzuku.
114
115. Mwenyezi Mungu akasema: Hakika Mimi nitakuteremshieni hicho.
Lakini yeyote katika nyinyi atakaye kanya baadae, basi hakika Mimi nitampa
adhabu nisiyopata kumpa yeyote katika walimwengu.
115
116. Na pale Mwenyezi Mungu atakapo sema: Ewe Isa bin Maryamu! Ati
wewe uliwaambia watu: Nifanyeni mimi na mama yangu kuwa ni miungu badala
ya Mwenyezi Mungu? (Na Isa) atasema: Subhanaka, Wewe umetakasika! Hainifalii
mimi kusema ambayo si haki yangu. Ikiwa nilisema basi bila ya shaka umekwisha
yajua. Wewe unayajua yaliyo ndani ya nafsi yangu, lakini mimi siyajui yaliyo
katika nafsi yako. Hakika Wewe ndiye Mjuzi mkubwa wa yaliyo fichikana.
116
117. Sikuwaambia lolote ila uliyo niamrisha, nayo ni: Muabuduni Mwenyezi
Mungu, Mola wangu Mlezi na Mola wenu Mlezi. Na mimi nilikuwa shahidi juu
yao nilipo kuwa nao. Na ulipo nifisha ukawa Wewe ndiye Muangalizi juu yao.
Na Wewe ni shahidi juu ya kila kitu.
117
118. Ukiwaadhibu basi hao ni waja wako. Na ukiwasamehe basi Wewe
ndiye Mwenye nguvu na Mwenye hikima.
118
119. Mwenyezi Mungu atasema: Hii ndiyo Siku ambayo wasemao kweli
utawafaa ukweli wao. Wao watapata Bustani zipitazo mito kati yake. Humo
watadumu milele. Mwenyezi Mungu amewawia radhi, nao wawe radhi naye. Huku
ndiko kufuzu kukubwa.
119
120. Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo.
Naye ni Muweza wa kila kitu.
120
Sura Nyingine | Faharasa |